
Wananchi wa kijiji cha Mukarazi kata ya Mabamba wilayani Kibondo mkoani Kigoma wameondokana na kutembea umbali wa zaidi ya kilomita 5 kufuata huduma sehemu zenye nishati ya umeme baada ya serikali kufikisha huduma hiyo kijijini humo
Baadhi ya wananchi hao akiwemo Ibrahim Emmanuel, Mugisha Bryson na Gaspari Ndaboroheye wamesema kwa sasa huduma mbalimbali zinapatikana ikiwemo mashine za kusaga mahindi zinazotumia mfumo wa umeme wa TANESCO, komputa pamoja na mashine za saluni za kunyolea nywele kwa kutumia umeme
Naye mwenyekiti wa kijiji cha Mukarazi bw. Ndinze Sebastian amesema wanaipongeza serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwafikishia huduma hiyo na kwa sasa zahanati ya kijiji hicho tayari inatumia komputa na huduma nyingine zinazohitaji nishati ya umeme
Amesema sehemu za kutolea huduma za kijamii ikiwemo Shule, zahanati, kituo cha polisi pamoja na ofisi za uhamiaji na mamlaka ya mapato TRA zimekuwa moja ya sehemu zilizopatiwa vipaumbele katika zoezi hilo la kuunganisha huduma ya umeme.